UTAFITI MBALIMBALI KATIKA DINI NA SAYANSI
IMEANDALIWA NA AL-AMIN ALI HAMAD
Mwenyeezi Mungu akipenda Mlango huu wa FIQH/TOHARA utakusanya Mafundisho ya Sala ya Imamu Shafii. Tafsiri Ya Kitabu Cha Abi Shujaa. Huu Ni mlango wa Pili. Mlango wa kwanza FIQH/TOHARA Ulimalizika na Ulikusanya Mafundisho ya Tohara. Nia yangu ni kufanya kazi hii kila siku kidogo kidogo. Na nitaweka Tarehe katika kila Darasa kama nilivyofanya leo tarehe 28/06/2022.
27/06/2022
Alhamdulilah Leo tutaanza safari yetu ya Kusoma mafundisho Ya Abi Shujaa ambaye nilimwelezea kwa kifupi katika mlango wa FIQH/TOHARA. Marehemu Abi Shujaa (Baraka za Mwenyeezi Mungu Mtukufu Zimfikie) alifanya kazi kubwa ya Kuandika Sheria za Elimu ya FIQH kwa njia ya kugawanya katika Mafungu na Milango mbalimbali baada ya kuitikia Mwito wa wanafunzi wake walipomuomba aiandike Elimu hii ya Imamu Shafii kwa njia iliyo Rahisi na Ya kueleweka.
Sheikh Abi Shujaa ameanza kuuelezea mlango huu kwa Kusherehesha “Nyakati Za Swala” kwa kusema
“Swala Tano Na Nyakati Zake”
Swala Ya Adhuhuri
Akaanza na Swala ya Adhuhuri kwa kusema “Swala ya Adhuhuri Ina Rakaa Nne. Na wakati wake wa kwanza ni Wakati Jua linapokuwa katikati wakati wa mchana na kisha likianza kutua. Yaani Jua linapokuwa katikati kisha pale likianza kuzama upande wa pili au kwa lugha nzuri pale linapoanza kusogea upande wa pili. kwa kiingereza Tutatumia Neno “Decline” Kwa kawaida wakati Jua likianza kusogea mbele hapo litasababisha Kivuli. Kwa hiyo kipindi hicho ndicho kinaitwa DHUHURI na mwisho wa kipindi hicho ni pale Kivuli cha kila kitu kifikie urefu sawa na Kitu hicho. Nadhani imeeleweka. Yaani kipimo cha Kivuli ya kila kitu kikiwa sawa na Urefu wa kitu hicho basi ujue Swala yeyote baada ya hapo itakuwa nje ya nyakati za Dhuhuri. Hiki ni kipimo kilichotumika hapo zamani enzi hizo wakati kulikuwa hakuna Saa na pia hata leo unapokua mbali na misikiti na pia ukiwa huna Saa basi tumia Jua kama tulivyosoma mafundisho ya Shafii yanayotokana na Hadithi za Mtume ﷺ Utaangalia Jua na Kipimo cha Kivuli. Kwa lugha Rahisi angalia Kivuli cha wakati wa Mchana. Urefu wa kivuli unapokuwa chini ya urefu wa kila kitu na hata kivuli chako mwenyewe basi huo ndiyo wakati wa Dhuhuri lakini unapozidi urefu wa chochote au hata kuvuli chako mwenyewe basi ujue Wakati wa Dhuhuri umepita.
Swala Ya Alasiri
Kwa hiyo Sheikh wetu anaendelea kuelezea Swala Ya AL-ASR kwa kusema “Swala ya Al-Asr ni Rakaa Nne” Na wakati wake ni pale Kivuli kinapozidi urefu wa kila kitu na hata kivuli chako mwenyewe. Ukisimama Nje katika jua angalia Kivuli chako mwenyewe ukiona urefu wa Kivuli umekupita basi ujue huo ndio mwanzo wa wakati wa Al-Asr. Na Sheikh Abu Shujaa anaendelea kusema kwamba Wakati unaopendeza kuswali Swala ya Al-Asr ni baada ya Kivuli cha urefu wa kila kitu kukizidi mpaka kufikia urefu mara mbili yake. Kwa mfano ukipima kivuli chako na ukiona urefu wa kivuli hicho kimefikia mara mbili ya urefu wako basi ujue wakati huo ndio karibu na mwisho wa Swala ya Al-Asr na baada ya urefu huo (wa Vivuli) inajuzu au inakubalika kuendelea kuswali Swala ya Al-Asr mpaka Jua litakapotua ijapokuwa siyo wakati Mzuri sana kama pale mwanzoni. Kwa hiyo Wakati wa Swala ya Al-Asr unaanza pale kivuli cha urefu wa jua kinapozidi urefu wako na wakati huo mzuri unaendelea kiasi cha kivuli kukifikia urefu wako au chochote kile mara mbili. Baada ya hapo (Urefu wa Vivuli mara mbili) inajuzu (inakubalika) kuswali Swala ya Al-Asr kabla ya Kuzama Jua. Ninapozungumzia Vipimo vya Vivuli ni kivuli cha kila kitu siyo kivuli chako tu. Kwa mfano kivuli cha nyumba, mawe, wanyama, na kila kitu. Nadhani imeeleweka.
Kwa Leo ninaishia hapa. Darasa lifuatalo litakuwa Swala Ya Maghrib, Ishaa na Asubuhi Mwenyeezi Mungu akipenda. Kesho Darasa Litaendelea Mungu akipenda….
28/06/2022
Swala Ya Maghrib
Swala Ya Maghrib Ni Rakaa Tatu na Wakati wake ni Wakati Jua Limetua au Kuzama. Baada ya Hapo katika Muda wa Nusu Saa ambao unatosha kwa Kufanya Adhana, Kufanya Udhu, KuKimisha Swala na Kuswali. Na kipindi hicho ni Mpaka Kabla Ya Adhana Ya Swala Ya Ishaa.
Swala Ya Ishaa
Swala Ya Ishaa Ni Rakaa Nne Na wakati wake wa mwanzo Mwanga wa Jua Mwekundu unapozama au kutoweka. Na Wakati wake unaendelea mpaka Theluthi Ya Usiku. Yaani Ugawe Usiku katika Mafungu Matatu kisha Fungu la kwanza. Kwa mfano Ukiwa Usiku ni Masaa Kumi Na Mbili basi Theluthi Ya Kwanza Ni Saa Nne Usiku. Na Pia Inajuzu kuswali Swala Hiyo wakati wowote baada ya wakati huo mpaka kabla Ya Alfajiri.
Swala Ya Asubuhi
Swala ya Asubuhi Ni wakati wa Alfajiri. Wakati wa Kiza na Mwanga. Yaani Katikati baina ya Kiza na Mwanga. Wakati huo unaendelea mpaka Mwanga unapolipunguza Kiza hilo. Yaani Mwanga unapoanza kuwa Mwingi kuliko Kiza. Na inajuzu (Inakubalika) baada ya Wakati huo kuswali katika Wakati kabla ya Kutoka Jua.
Kwa Leo ninaishia hapa. Darasa lifuatalo litahusu Masharti ya Kuwajibika kwa Swala na Swala Za Sunna. Mwenyeezi Mungu akipenda.
Darasa Litaendelea Mungu akipenda….
SHURUTI ZINAZOWAJIBIKA KATIKA SWALA
SWALA ZA SUNNA